BIBLIA INAJIBU: NANI ANAYEPASWA KUPIGA GOTI WAKATI WA KUVISHA PETE YA UCHUMBA? |BY PRINCE BEWISA - Fahamu zaidi Staili za Maisha na Saikolojia. Bewisa App | ™ - Efe. 5:15-17
SOMA HIZI PIA:
Loading...

BIBLIA INAJIBU: NANI ANAYEPASWA KUPIGA GOTI WAKATI WA KUVISHA PETE YA UCHUMBA?



UNAWEZA KUPATA STORI ZETU MOJA KWA MOJA KWA KUBONYEZA 'LIKE' HAPA



« Piga 0652262137 kuweka tangazo lako hapa - Push kwa Buku tu »

 

Na; Mw. Benson Mmari 

Miongoni mwa mambo tata kwenye jamii ni suala hili, yaani nani anapaswa kupiga goti wakati wa kuvisha pete ya uchumba? Kumekuwa na mjadala mkubwa sana juu ya jambo hili na majibu ni mengi lakini kwa bahati mbaya wengi wanatoa majibu kulingana na mapokeo ya wazungu au pia utamaduni wa kabila lake, utashi na hata namna alivyolelewa hasa mfumo wa familia yake katika kuheshimu jinsia.

Nimezungumza “kupiga goti” hapo juu na sio magoti. Kupiga goti kwanza ujulikane ni umoja na si wingi; hii ikiwa na maana ya kuwa haijalishi ni nani anatakiwa kutekeleza hicho kitendo kati ya mwanaume au mwanamke, bado inatakiwa tafsiri ijulikane kwanini unafanya hivyo. Kwanza hutakiwi kupiga magoti yote mawili. Kumbuka kupiga magoti ni ishara ya kunyeyekea kwa aliyekuzidi nafasi. Kwa lugha nyingine ni kama kusujudu.

Katika utamaduni wa Kiyahudi na Kibiblia pia, anayepaswa kusujudiwa ni Mungu peke yake; lakini hii haina maana kuwa kupiga magoti mbali na mbele ya uso wa Mungu haitakiwi isipokuwa iwe na tafsiri ya kutosujudia hicho kitu kiasi cha kuichukua nafasi ya Mungu kwenye maisha yako. Kiyahudi aliyetakiwa kupigiwa magoti mbali na Mungu ni mtu mwenye cheo kikubwa, mfano mtumwa mbele ya bwana wake; huyu alipiga magoti na kumbusu bwana wake miguu. Hata hivyo ishara ya kuheshimu inaoneshwa pia kwa wanaolingana vyeo ambao wao hawakupigiana magoti isipokuwa walipeana busu mashavuni.

Kitendo cha kupiga goti kwa mguu mmoja kilionekana kwa watumishi ambao wanafanya kazi ya Mungu pamoja lakini mmoja akiwa kwenye nafasi ndogo (junior minister) basi alitakiwa kumsujudia mwenye nafasi kubwa (senior minister) walipokutana na kusalimiana ili kufanya huduma pamoja. Na hii inaonekana mpaka leo hasa kwa dhehebu la Roman Catholic na kidogo Lutheran ingawa wao hawapigi goti bali aliye mdogo husuka kidogo madhabahuni au kusogea mbele kidogo ya kuhani mkuu hasa wakati wa kutoa Baraka za Utume mwisho wa Ibada.

Sasa basi, kwa mtindo huu huu wa kuhani mkuu na mdogo kwenye huduma ndio huo huo unaotakiwa kuchukuliwa kwenye uchumba. Nasema hivi kwa sababu kwenye ukuhani wote bila kujali ukubwa au udogo kwa Mungu ni Makuhani na wapo sawa isipokuwa kibinadamu wanaoneshana heshima na si kuabudiana. Kadhalika na kwenye uchumba, ingawa kuna tofauti kidogo ambayo hiyo tofauti itaegemea kwenye jinsia ipi ipige goti na hapo ndipo yalipo majibu.

Tunaamini kwamba mpaka wawili wakutane na kuvisha pete kuna mkono wa Mungu umehusika ingawa si lazima iwe hivyo japo inatakiwa iwe hivyo. Nazungumza kwa wale ambao Mungu ameamua kuwakutanisha kama mume na mke mwema. Kama ni hivyo, hawa ni kama makuhani na katika hao mkubwa na mdogo hapimwi kama kuhani wa madhabahu (ambao wanapimwa kulingana na elimu ya kuhani au nafasi yake kwenye kanisa bila kujali jinsia yake). Hawa (wenzi) wanapimwa kwa jinsia kulingana na mpangilio wa majukumu Kimungu kati yao.

Kwa mujibu wa Biblia, ni dhahiri na tutakubaliana kwamba Mungu aliwaumba mwanaume na mwanamke pamoja kwenye mawazo yake, lakini kiuhalisia alianza kumuumba mwanaume kwanza kisha baadae ndipo alipokuja kumuumba mwanamke kutoka kwenye ubavu wa mwanaume. Hii tunaipata tunaposoma Kitabu cha Mwanzo sura ya kwanza na ya pili.

Biblia pia inaeleza kuwa mwanamke aliumbwa kwa ajili ya mwanaume, lakini mwanaume aliumbwa kwa ajili ya Mungu na kamwe si kwa ajili ya mwanamke (1Kor. 11:9). Na pia mwanamke alihukumiwa kuwa chini ya mwanaume na kutawaliwa na mwanaume (Mwanzo 3:16).

NUKUU ZA BIBLIA:

Maana mwanamume hakutoka katika mwanamke, bali mwanamke katika mwanamume. Wala mwanamume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamke, bali mwanamke kwa ajili ya mwanamume. – 1WAKORINTHO 11:8-9

Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala. – MWANZO 3:16

Baada ya kutazama nafasi ya mwanamke na mwanaume hebu tutazame majukumu yao wanapokuwa pamoja kwa kuunganishwa na upendo. Katika hili mwanaume amepewa jukumu la kumpenda mwanamke na mwanamke yeye amepewa kumtii mwanaume. Kutii ni kunyenyekea na kufuata lile ambalo utaagizwa. Sasa si mpaka aelekezwe jambo, lakini mwanamke anatakiwa kila wakati kuonesha namna anavyomheshimu mwanaume na mwanaume anatakiwa kufanya kila njia kumwonesha mwanamke kuwa anampenda kwa vitendo na hata kauli. Kupenda si kunyeyekea, kupenda ni kupenda na sifa za upendo zipo kwenye 1Wakorintho 13. Hapo naomba tuelewane, hahahahaha (nacheka kidogo). Hebu turejee Maandiko tena:

Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; - WAEFESO 5:22,23,25

Baada ya hayo tutazame tena ni nani anakuja kwa mwenzake, ni mwanaume anakwenda kwa mwanamke ama ni mwanamke anakwenda kwa mwanaume? Hapa niseme wazi kuwa wanakutana (hahahahaha, nacheka tena). Na katika hili si mawazo yangu bali Biblia inasema, “Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” (Mt. 19:4-6)

Hapo kwenye nukuu ya Biblia ni wazi kwamba inasema zaidi juu ya mwanaume kuanza kuondoka. Inaposema “ataambatana na mkewe” ina maana kwamba huyu mwanamke lazima awe ametoka kwao pia kwa hiyo wanakutana na kuwa mwili mmoja. Kwanini nimegusa hili? Ni kwa sababu wapo watu wanaodhani kwamba wanawake hufuatwa, ni kweli hufuatwa lakini na yeye pia hutoka na kuitikia wito wa kufuatwa. Na kule kufuatwa tu kwa maana ya mwanaume kuanza kuonesha kumchagua huyu mwanamke, basi ni heshima kubwa sana huyu mwanamke anakuwa ametendewa na huyu mwanaume kwa maana mwanamke ni kwa ajili ya mwanaume na mwanaume kwa ajili ya Mungu hivyo ni kama upendeleo fulani huyu mwanamke anakuwa ametendewa. Na ndio maana Biblia kwenye Kitabu cha Isaya inaita kitendo hiki kama kusitiriwa aibu (Isaya 4:1).

Mwanamke asipofuatwa na mwanaume ili kuolewa, Biblia inatafsiri kwamba huyu mwanamke ni kama yupo kwenye aibu. Hivyo mwanaume anapomfuata ili kutaka kumwoa basi anakuwa amekuja ili kumsitiri aibu yake. Sasa unaweza kujiuliza; kati ya msitiri aibu na msitiriwa aibu ni nani yupo juu ya mwenzake? Hakika ni msitiri ambaye ni mwanaume. Na ndio maana Biblia inasema kwamba itatokea nyakati wanaume watakuwa wachache, na ikiwa itatokea mwanamke hajasitiriwa (hajaolewa sasa), itafika wakati wanawake saba watamwendea mwanaume mmoja na kujigharamia kila kitu ili mradi tu aitwe kwa jina la huyo mwanaume na kusitirika aibu yake. Kwa maana hiyo mwanaume anakuwa kitu cha thamani sana kwa mwanamke:

Na siku hiyo wanawake saba watamshika mtu mume mmoja wakisema, Tutakula chakula chetu, na kuvaa nguo zetu wenyewe, lakini tuitwe tu kwa jina lako; utuondolee aibu yetu. – ISAYA 4:1

Ninaposema hizi hoja silengi kumnyanyapaa mwanamke hata kidogo, hapa tafadhali nieleweke vema kabisa. Najua wanawake ni jeshi na mashujaa sana tena wenye uwezo mkubwa na ndio maana wakawekwa kama wasaidizi, maana hakuna msaidizi ambaye ni dhaifu, lazima awe na nguvu na uwezo kuliko anayesaidiwa. Tena wanawake wamewekwa pia makusudi ili kuwalinda wanaume. Biblia inasea kwenye Yeremia 31:22b kuwa, “Kwa maana Bwana ameumba jambo jipya duniani; mwanamke atamlinda mwanamume.”  Tena hawa wanawake ndio watu wa kwanza kueneza Habari Njema ya kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo, hivyo si viumbe vya mchezo mchezo. Lakini pamoja na hayo, tunaangalia nafasi kati ya mwanaume na mwanamke wanapokuwa pamoja, Mungu ameweka utaratibu gani? Hapo ndipo tunaona Mungu amempa mwanaume majukumu mengi zaidi kuliko mwanamke na hii inatoa pia fursa ya mwanaume kuwa juu ya mwanamke lakini kwa kumpenda, kumthamini na kumchukulia kama chombo dhaifu. Biblia inaongeza hivi, “Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” – 1PETRO 3:7

Kwa hoja hizo hapo juu, ni wazi sasa umepata jibu kwamba ni nani anapaswa kupiga goti wakati wa kuvisha pete ya uchumba. Kama bado nikuambie kuwa ni MWANAMKE NDIYE ANAYEPASWA KUPIGA GOTI WAKATI WA PETE YA UCHUMBA kwani kwa kufanya hivyo atakuwa anaonesha utii na heshima kwa mwanaume ili kutimiza jukumu lake la kwenye Biblia.

Asante, naitwa Mw. Benson Mmari

Ikiwa kuna maswali zaidi, wasiliana name kwa WhatsApp na. +255 652 262 137

Ili kupata Makala zaidi na kwa njia rahisi, Install App yetu kwenye PlayStore. Tafuta BEWIS APA, au BONYEZA HAPA



TUAMBIE UNA MAONI GANI JUU YA HILI?

Facebook Plugin by princebewisa

Chapisha Maoni

Enenda kwa hekima, ukijua ni yapi yaliyo mapenzi ya Mungu huku ukiukomboa wakati. Install Bewisa App kwenye PlayStore kwa maarifa zaidi.
- EV. BENSON W. MMARI, +255 768 111 279

CodeNirvana
© Copyright Bewisa App | ™ - Efe. 5:15-17 | Modified By PB Web and Graphics
Back To Top